TANGAZA NASI HAPA

Wednesday, 8 March 2017

Yanga SC vs Zanaco FC ; Hizi ndizo changamoto anazokabiliwa nazo Lwandamina,ni lazima kufuzu….



 Na Baraka Mbolembole

BAADA ya kuvuka  hatua ya awali kwa ushindi wa jumla ya magoli 6-2 dhidi ya Ngaya Club kutoka Comoro,mabingwa wa kihistoria wa ligi kuu ya Tanzania Bara-Yanga SC siku ya Jumamosi hii watarejea uwanjani kucheza dhidi ya mabingwa wa Zambia,Zanaco FC katika mchezo wa raundi ya mwisho kabla ya kufuzu kwa hatua ya makundi-Caf Champions league 2017.

Ni mechi nyingine ngumu kwa kikosi hicho kilichoshinda mataji 25 katika ligi ya Bara. Ikiwa na kumbukumbu ya kufika hatua ya makundi mara moja mwaka 1998, hakika miaka karibia 20 sasa Yanga wanakidhi viwango vya kuvunja rekodi yao hiyo na kufuzu kwa mara ya pili makundi ya ligi ya mabingwa Afrika-michuano mikubwa zaidi ya vilabu barani Afrika.



ILIPOTOKA MIAKA 18 ILIYOPITA…..

Yanga ‘ilibatizwa’ jina la ‘Jamvi la Wageni’ baada ya kupokea vipigo vya  6-0, 4-0 ilipofuzu kwa mara ya kwanza hatua ya makundi katika ligi ya mabingwa mwaka 1998. Vipigo hivyo vilitoka kwa Raja Casablanca ya Morocco  na Maning Rangers  ya Afrika Kusini na walimaliza mechi sita za makundi wakiwa na alama mbili tu, baada ya kuambulia sare Dar es Salaam dhidi ya Raja na Asec Mimosas ya Ivory Coast.

Tangu wakati huo imefanikiwa kushinda mataji tyisa ya ligi kuu Tanzania Bara ( 2002, 2005, 2006, 2007/08, 2008/09, 2010/11, 2012/13, 2014/15, 2015/16,) imeshinda mataji mawili ya klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati ( 2011 na 2012,) pia wameshinda mataji ya Ngao ya Jamii na FA Cup ndani ya Tanzania bara.

Hii inamaanisha wameendelea kujiimarisha katika soka la ndani, hivyo wanapaswa kutumia uzoefu na mafanikio yao hayo kuifunga Zanaco timu ambayo imeshinda ubingwa wa ligi kuu Zambia mara Saba tu huku wakifanya hivyo ndani ya miaka hii 15 (2002, 2003, 2005, 2006, 2009, 2012, 2016)

Mafanikio makubwa ya timu hiyo ya Zambia katika ligi ya mabingwa ni kufika hatua ya 16 bora na walifanya hivyo mwaka 2010 walipocheza kwa mara ya tano ya mwisho.

Mwaka 2003 walicheza kwa mara ya kwanza michuano hiyo ya mabingwa na kuishia raundi ya kwanza, wakarejea tena mwaka 2004 safari hii waliishia raundi ya pili baada ya kuwaondoa Simba SC ya Tanzania bara katika raundi ya kwanza kwa jumla ya magoli 2-1.

Miaka ya 2006 na 2007 waliishia raundi ya kwanza kabla ya kufikia mafanikio yao ya juu zaidi katika michuano ya mwaka 2010 ambako waliondolewa hatua ya 16 bora na kuangukia katika michuano ya Caf Confederation Cup ambako walifanikiwa kufuzu kwa hatua ya makundi.

Kwa kutumia uzoefu wa kushiriki mara ya 22 sasa michuano ya mabingwa Afrika,naamini Yanga hawapaswi kuidharau hata kidogo Zanaco lakini ni lazima waitumie kama ‘ngazi’ ya kupandia kwenye kilele cha mafanikio. Yanga wana uzoefu wa kutosha sasa wa kuwaondoa timu hiyo iliyoanzishwa mwaka 1985

Yanga wanacheza michuano yao ya tisa ya klabu bingwa tangu walipofuzu kwa mara ya mwisho hatua ya makundi,na mara tatu wamefanikiwa kufika hatua ya mwisho kabla ya kufuzu kwa hatua ya makundi. Walifanya hivyo miaka ya 2001, 2007 na 2016.



NI WAKATI WA WACHEZAJI WA KIGENI ‘KUULIPA’ MPIRA WA TANZANIA
 Mlinzi wa kati raia wa Togo, Vicent Bossou, viungo Mzimbabwe, Thaban Kamusoko, Mnyarwanda,Haruna Niyonzima, Mzambia,Justine Zulu na washambuliaji,Mzambia,Obrey Chirwa, Mrundi,Amis Tambwe na Mzimbabwe, Donald Ngoma wameshafanya kazi nzuri ndani ya kikosi cha Yanga.

 Ukiachana na Wazambia, Zulu na Chirwa, wachezaji hao wengine wa kigeni walikuwepo katika kikosi cha timu hiyo kilichoshinda mataji ya FA Cup na ligi kuumsimu uliopita,na walikuwa sehemu ya timu iliyotolewa hatua ya 16 bora katika ligi mabingwa Afrika na Al Ahly ya Misri kwa jumla ya magoli 3-2 na kungukia katika Confederation Cup ambako walifanikiwa kufika hatua ya makundi kwa mara ya kwanza.

Hakika wachezaji hao wa kigeni walikuwa na mchango mkubwa sana katika msimu wao wa kwanza klabuni Yanga,na hilo ndiyo lilichochea Chirwa kusajiliwa kwa thamani isiyopungua milioni 200 kutoka Platnum FC ya Zimbabwe naa kuweka rekodi ya mchezaji ghali zaidi katika soka la Tanzania.

Kama klabu inatumia hadi milioni 200 kumsaini mchezaji wa kigeni na kumlipa mshahara usiopungua milioni 8 kwa mwezi bila shaka inataraji makubwa zaidi kutoka kwa mchezaji husika na kwa Yanga sasa wana kiu kubwa ya kuhakikisha wafuzu kwa hatua ya makundi katika michuano ya ligi ya mabingwa.

Ili jambo hilo liwezekane kila mchezaji anapaswa kujituma,kuwa na nia na utayari wa kupambana kuhakikisha hilo linatokea.

Ukitazama katika kikosi cha Yanga kuelekea mchezo wa Jumamosi hii dhidi ya Zesco utagundua kuwa kocha Mzambia,George Lwandamina na wasaidizi wake Juma Mwambusi na Juma Pondamali wanakabiliwa na changamoto ya kutengeneza timu mpya kutoka katika kikosi kile kilichokuwa chini ya kocha aliyepita Mholland,Hans van der Pluijm.

Na mabadiliko hayo yanapaswa kufanyika si kwa kupenda bali kutokana na maumivu ambayo yamekuwa kwa baadhi ya wachezaji wa kikosi cha kwanza kama beki namba mbili,Juma Abdul, Niyonzima,Kamusoko, Ngoma na Tambwe. Hawa ni wachezaji watano ambao wameifikisha Yanga hapo ilipo,na sasa jambo la kujiuliza je, wachezaji  wengine wanaweza kupigana na kuziba mapengo ya wachezaji hao?

Hassan Kessy nimzuri sana katika ushambuliaji, lakini tatizo lake kubwa ni kupenda kuuchezea sana mpira na kukimbia nao. Tofauti na Juma Abdul ambaye yeye hushambulia sana kwa kutegemea uwezo wake wa kupiga krosi za mbali na pasi zinazofika.

Mechi za kimataifa ni ngeni kwa Kessy na endapo atapewa nafasi ningependa acheze kwa umakini kama anavyofanya Juma na asipendeleee sana kukimbia na mpira hadi katika lango la wapinzani kwa sababu jambo linaweza kutoa ‘mwanya’ kwa Zanaco na kutumia mipira ya ‘kustukiza’ kupitia upande wake.

Atapaswa kushambulia lakini asijisahau kurejea haraka katika nafasi yake. Naamini Kessy anaweza kuleta uwiano usiopishana sana na Juma Abdul katika beki namba mbili ikiwa Juma atashindwa kurejea katika mchezo huo.

Ni ngumu sana kuziba mapengo ya Thaban na Niyonzima kwa aina ya wachezaji waliopo sasa katika timu ya Yanga, lakini ikitokea wawili hao kukosekana hakuna namna itawabidi benchi la ufundi kuwaandaa Said Juma Makapu, na Juma Mahadhi ambaye alipata majeraha pia katika mchezo wa FA Cup siku ya Jumanne hii dhidi ya Kiluvya United.

Kiukweli bila ‘ma-pro’ hao katikati ya uwanja Yanga watapa shida kupata matokeo japokuwa watakuwa nyumbani,hasa ukizingatia Zulu ambaye alisajiliwa kwa matarajio makubwa akiwa bado hajatulia huku akionekana kuwahi kuchoka mchezoni.

Licha ya kufunga magoli 14 hadi sasa katika michuano yote, Chirwa ni mchezaji ambaye anahitaji msaada wa Ngoma au Tambwe ili kuendelea kufunga magoli. Uwezo wa chini kutoka kwa Malimi Busungu katika mchezo wa ligi kuu dhidi ya Mtibwa Sugar wikendi iliyopita ni kielelezo tosha kuwa mchezaji huyo si wa kumtegemea kuibeba timu katika mchezo dhidi ya Zanaco.

EmmanuelMartin bado anaendelea kujipambanua hivyo kuwakosa Tambwe na Ngoma ni ‘jambo baya’ kwa Yanga kuelekea mchezo wa Jumamosi hii ambao ni muhimu kushinda. Kama wachezaji hao wa kigeni watakuwepo basi huu ni wakati wao wa kuilipa Yanga na kuifikisha hatua ya makundi katika ligi ya mabingwa Afrika.



TATIZO LA SAFU YA ULINZI….
 Udhaifu mkubwa wa kikosi cha Yanga lipo katika eneo la ulinzi,japokuwa wanaonekana kuwa na wachezaji wazuri,lakimni ukweli maelewano ya walinzi wa kati si mazuri, na hilo ndilo lilichangia ‘maumivu’ ya kufungwa 4-0 na Azam FC katika michuano ya Mapinduzi Cup hata katika michezo dhidi ya Mbeya City FC, Simba SC na Tanzania Prisons tatizo hilo liliwangusha.

Unapokuwa na kipa bora kama Deogratius Munish ‘Dida’ unatakiwa kufanya makosa makubwa katika beki ili kuruhusu nyavu zako kufikiwa na mpira mara kwa mara na hilo ndilo limekuwa likifanya na walinzi wa kati wa Yanga. Iwe,Bossou na Kelvin Yondan, Nadir na Bossou,Nadir na Kelvin,Vicent Andrew na Bossou,Andrew na Kelvin au Nadir na Andrew.

Wanashindwa kuwa na maelewano mazuri ndiyo maana wamekuwa wakiruhusu goli katika michezo mingi hivi sasa-hata dhidi ya Kiluvya, Ngaya ambazo ni timu dhaifu. Andrew bado kijana na anachipukia vizuri lakini uzoefu alioupata Mtibwa Sugar bado haujadhihirisha ubora wake katika kikosi cha Yanga, wazoefu Kelvin, Nadir na Bossou wote wamekuwa wakijichanganya na kuruhusu Dida kuwa matatizoni mara kwa mara.

Kuanzia katika beki za pembeni,Kessy/Abdul katika beki namba mbili,Mwinyi Hajji na Oscar Joshua katika beki namba tatu hadi kwa walinzi wa kati Yanga wanapaswa  kuongeza uwezo wao wa kiutulivu, kimbinu na kiakili. Hii ni nafasi yao ya wazi kufuzu kwa hatua ya makundi.

No comments:

Post a Comment