TANGAZA NASI HAPA

Saturday, 4 March 2017

VPL: Ushindi wowote kuirudisha Yanga kileleni leo, Chirwa kuivaa Mtibwa


 
 MABINGWA watetezi wa ligi kuu ya kandanda Tanzania bara, timu ya Yanga SC leo itakuwa na kibarua kigumu ugenini Jamhuri Stadium, Morogoro itakapowakabili Mtibwa Sugar FC katika muendelezo wa michezo ya ligi kuu ya Vodacom.


 Yanga inashika nafasi nyuma ya vinara Simba SC na ushindi wa aina yoyote katika mchezo wa leo utawapeleka kileleni kutokana na wastani wao mzuri wa magoli ya kufunga na kufungwa.

 Baada ya kulazimishwa sare ya kufungana 2-2 na Mbeya City FC siku ya jana Jumamosi, Simba wanaongoza ligi wakiwa na alama 55(pointi 3 mbele ya Yanga wanaoshika nafasi ya pili.)

Ushindi katika uwanja wa Jamhuri leo kwa kikosi cha kocha Mzambia, George Lwandamina utawafanya mabingwa hao watetezi kurejea kileleni kutokana na wastani wao mzuri wa magoli.


 Katika michezo 24 waliyokwishacheza Simba imefanikiwa kufunga magoli 40 na kuruhusu nyavu zao mara kumi hivyo kuwa na wastani wa magoli 30, wakati Yanga katika michezo 23 waliyokwishacheza wamefanikiwa kufunga magoli 49 na kuruhusu magoli 11 hivyo kuwa na wastani wa magoli 38.

 Yanga imefanikiwa kushinda mara moja tu katika uwanja wa Jamhuri tangu mwaka 2009 dhidi ya Mtibwa huku ushindi wao pekee ukiwa ule wa 2-0 katika mchezo wa raundi ya kwanza msimu uliopita.

Mshambuliaji Mzambia, Obrey Chirwa ambaye alioneshwa kadi nyekundu ya utata katika mchezo wa Jumatano iliyopita vs Ruvu Shooting amefutiwa adhabu hiyo na Kamati ya masaa 72 hivyo atawavaa Mtibwa katika mchezo wa leo.


 ' Wakata miwa' hao wa Turiani, Morogoro wapo nafasi ya tano katika msimamo wakiwa na pointi 33 baada ya kucheza michezo 23.

 Mchezo mwingine leo Jumapili utapigwa katika uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam utazikutanisha African Lyon iliyo nafasi ya 14 na pointi 23 dhidi ya Mwadui FC iliyo nafasi ya 6 na alama 31.

No comments:

Post a Comment